Na James Timber, Mwanza

Jeshi la Polisi Wilaya ya Sengerema Mkoa wa Mwanza limetia mbaloni Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Luchili iliyoko Kata ya Nyanzenda  Halmashauri ya Buchosa Wilayani  Sengerema Mkoa wa Mwanza  Joshua Nyaombo kwa tuhuma za  kumpatia ujauzito mwanafunzi wake  jina limehifadhiwa anayesoma darasa la saba kwenye shule hiyo.

 Mkuu wa Polisi Wilaya ya Sengerema Maili Makoli alisema tayari watumiwa wawili wamekamatwa na jeshi la polisi  kwa tuhuma hiyo ikiwemo kumtorosha mwanafunzi huyo ili kuficha ukweli na uchunguzi unaendelea.

Aliwataja wahumiwa waliokamatwa kuwa ni mwalimu mkuu wa shule ya msingi Luchili Joshua Nyaombo anayetumiwa kumpatia ujauzito mwanafunzi huyo na mama mzazi wa mwanafunzi huyo Elizabeth  Busumabu anayedaiwa kushirikiana na mwalimu kumtorosha binti huyo.

Tuhuma za mwalimu huyo zimekuja baada ya wananchi kulalamika suala hilo ambalo limezua mjadala mkubwa kwenye jamii licha ya viongozi wa elimu ngazi ya Kata kulifahamu na kisha kulifumbia macho na kuacha jamii ikilalamika.

Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Luchili Mariahida Santrunini alisema kuwa jamii ya kijiji hicho imekuwa ikimlalamikia mwalimu huyo kufanya vitendo visivyo na staha na huku yeye ni kioo cha jamii na kumutaka aondolewe kwenye kijiji hicho.

Kuhusu suala la kutuhumiwa kumpatia ujauzito  mwanafunzi wake Afisa Mtendaji wa Kijiji hicho Mariahida Santrunini alikiri kuwa ni kweli alitenda kosa hilo kutokana na jamii hiyo kuthibitisha alimpatia ujauzito mwanafunzi wake kisha kupanga njama za kumtorosha yeye na mama  wa binti huyo ili kuficha ukweli wa jambo hilo.

Mwalimu Mkuu huyo Joshua Nyaombo amekuwa na matukio na tabia zisizo faa baada ya kufumaniwa akifanya kitendo cha ngono na binti wa kazi wa afisa mtendaji wa kijiji cha Luchili  alipokwenda nyumbani hapo kuchaji simu yake wakati afisa mtendaji akiwa kazini.

Mariahida Santrunini ambaye ni afisa mtendaji wa kijiji cha Luchili alisema kuwa   mwalimu huyo anapaswa kuchukuliwa hatua kutokana na  vitendo vyake vimewakela wananchi baada ya kumfumania akifanya vitendo vya ngono na binti yangu  wa kazi nyumbani kwangu wakati nikiwa kazini.

"Kweli mwalimu alimpatia ujauzito mwanafunzi wake lakini  suala hilo halijalipotiwa kwenye ofisi yangu , mimba iliyoripotiwa ni ya mtu mwingine jambo hili linashangaza mamlaka husika zinatakiwa kuwajibisha,’’ alisema  Santrunini.

Baba mzazi wa mwanafunzi huyo Charles Kanyenyera alisema hana taarifa yoyote juu ya binti yake anachofahamu yeye binti yake anasoma na anashangazwa na taarifa hizo.

"Mwandishi mimi nashangaa kwanza wewe ndiyo wa kwanza kunipatia taarifa mama yake tulitengana nikamuachia mji nasikitika sana juu ya hili ni kitendo cha kinyama lazima nifuatilie,’’  alisema  Kanyenyera.

Mmoja wa wananchi wa kijiji hicho Juma Ntalita alisema matukio ya wanafunzi kupatiwa ujauzito  yamekithiri kwenye shule hiyo mwalimu mkuu huyo ni kweli amempatia mimba mwanafunzi wake hivyo anatakiwa akamatwe ili aseme ukweli licha ya mwanafunzi huyo kutoroshwa.

Mwalimu mkuu shule ya Msingi Luchili anayetuhumiwa kumpatia ujauzito mwanafunzi wake Joshua Nyaombo alipoulizwa na waandishi wa habari ofisini kwake  alikana kufanya tendo hilo na anachofahamu mwanafunzi huyo ni mtoro.

"Mimi sijafanya kitendo hicho mwanafunzi huyo ni mtoro aliacha kuja shule tangu Mwezi Aprili 30, mwaka huu hadi sasa na sijui yuko wapi," alisema  Nyaombo.

Elizabeth Busumabu ni mama mzazi wa binti aliyepewa ujauzito alipozungumuza na mwananchi  alisema binti huyo alitoroka nyumbani na kwa sasa hafahamini aliko na wala hajui kama ana ujauzito na  yeye anasikia maneno hayo kwa watu.

Kaimu Afisa Elimu Kata ya Nyanzenda Maketa Makweba alisema suala hilo analifahamu na alikwisha mwita mwalimu huyo ili amwambie ukweli lakini alikana kutenda kosa hilo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Buchosa Crispin Luanda alipoulizwa juu ya suala hilo alisema hana taarifa na ameahidi kulifuatilia na itakapo bainika atachukuwa hatua.

Aidha, Mkuu wa Wilaya ya Sengerema Emmanuel Kipole alisema licha ya kusema hana taarifa alisikitishwa na kitendo cha mwalimu huyo na kusema kuwa hatua kali zitachukuliwa dhidi yake.

Post a Comment

Previous Post Next Post