Walinzi wa pwani nchini Libya wamesema jana wamewakamata wahamiaji karibu 40 ambao walikuwa wanaelekea Ulaya nje ya pwani ya bahari ya Mediterania na kuwapeleka katika vituo vya kuwashikilia ambavyo vilishambuliwa mapema mwezi huu.

Msemaji wa kikosi hicho cha walinzi wa pwani Ayoub Gassim amesema boti ya mpira iliyokuwa imewachukua wahamiaji 38, wengi wao wamisri, ilizuiwa siku ya Jumanne nje ya pwani hiyo kiasi ya kilometa 65, mashariki mwa mji mkuu, Tripoli.

Amesema wahamiaji walihamishiwa katika kituo cha kuwashikilia cha Tajoura. Umoja wa Mataifa umeeleza wasi wasi wake mkubwa jana kuwa wahamiaji hao wapya wamepelekwa Tajoura, ambako shirika la kuwahudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa linakadiria kuwa wakimbizi 200 na wahamiaji wanashikiliwa hapo.

Post a Comment

Previous Post Next Post