KIKOSI cha kocha Jurgen Klopp (pichani) “kimekuwa si cha kawaida” baada ya kukamilisha kalenda ya mwaka bila ya kufungwa hata mchezo mmoja katika mbio za kuwania ubingwa wa Ligi Kuu ya England.

Liverpool juzi iliibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Sheffield United na kuifanya timu hiyo kuendeleza wimbi la kutofungwa hadi sasa. Kikosi hicho cha Klopp kimerejea katika tofauti ya pointi 13 dhidi ya timu ya Leicester iliyopo katika nafasi ya pili, shukrani kwa mshambuliaji wa kimataifa wa Misri, Mohamed Salah na Msenegali Sadio Mane katika mchezo huo uliopigwa Anfield.

Huo ni ushindi wa 19 wa Liverpool kati ya mechi 20 ilizocheza za Ligi Kuu ya England msimu huu ikikamilisha miezi 12 ya timu kuwa kileleni. Timu hiyo haijapoteza mchezo wowote kati ya 37 ya Ligi tangu ilipofungwa na Manchester City Januari 3, 2019 na inaonekana kama itatwaa ubingwa kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1990. Huku ikiwa na mchezo mmoja mkononi, timu hiyo imeendeleza ubabe wake wa kuendelea kujikita kileleni katika mbio hizo za kuwania taji hilo.

“Kuna mambo mazuri mengi. Sina maneno ya kuzungumza, ni ya kipekee,’’ alisema Klopp. “Kwa kweli ni furaha sana na ninajivunia vijana wangu. Kamwe hatutachukulia mambo kwa wepesi.”

Washindi hao wa mechi 18 za nyumbani za ligi, Liverpool haijafungwa katika mechi 51 kubwa kwenye uwanja wao wa Anfield ukirejea nyuma hadi Aprili mwaka 2017.

Post a Comment

أحدث أقدم